Advert enquiry : ajirayako@gmail.com

JKT National Service

Follow

JKT National Service

(0)

About Us

JKT National Service

Miaka 51 iliyopita, yaani tarehe 10 Julai 1963 Jeshi la Kujenga Taifa lilianzishwa rasmi kufuatia utekelezaji wa Azimio la Kikao cha Baraza la Mawaziri. Kikao hicho kilifanyika tarehe 19 Aprili, 1963 chini ya uongozi wa Amiri Jeshi Mkuu na Rais wa Tanganyika hayati Mwalimu Julius Nyerere.

Wazo la kuanzishwa kwa JKT lilitokana na mapendekezo ya Mkutano Mkuu wa Umoja wa Vijana wa Chama cha Tanganyika African National Union (TANU Youth League), Mkutano uliofanyika mkoani Tabora mwaka 1958 ambalo lilitolewa na Katibu Mkuu wa TANU Youth League wakati huo Ndugu Julius Nyerere, ambaye sasa ni marehemu.

Sheria Iliyoanzisha JKT

Jeshi la Kujenga Taifa lipo kisheria, kwa vile ilipofika mwaka 1964, Bunge lilitunga Sheria ya kuanzishwa kwa JKT na sheria hiyo iliupa nguvu ya kisheria uamuzi wa mwaka 1963 wa Baraza la Mawaziri wa kuanzishwa kwa Jeshi hilo.

Kwa mujibu wa Sheria ile, kujiunga na JKT ilikuwa jambo la kujitolea. Mwaka 1966 sheria hiyo ilifanyiwa marekebisho na kuanzisha utaratibu wa kujiunga JKT kwa mujibu wa Sheria.

Utaratibu huu uliwahusu vijana waliohitimu vyuo vikuu, vyuo vya elimu ya juu, kidato cha sita na waliomaliza kidato cha nne ambao wamepata mafunzo kwenye vyuo vya taaluma mbalimbali kama vile ualimu, uganga, uuguzi na kadhalika.

Mkurugenzi wa JKT aliwezeshwa kisheria kuwaita vijana hao kujiunga na JKT.Mwezi Julai 1967, kikundi cha kwanza cha vijana wasomi 64 kilijiunga na JKT katika Operesheni Azimio.

Katika kuunga mkono uamuzi wa Serikali kuhusu kuanzishwa kwa Jeshi la Kujenga Taifa, viongozi na wasomi wengine waliohitimu zamani waliamua kujiunga na mafunzo ya JKT. Kwa mfano aliyekuwa Makamu wa Pili wa Rais Mheshimiwa Rashid Kawawa, aliyekuwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais Mheshimiwa Aboud Jumbe, aliyekuwa Spika wa Bunge Chifu Adam Sapi Mkwawa pamoja na baadhi ya Wabunge na viongozi mbalimbali wa Chama na Serikali walijiunga na mafunzo ya Jeshi la Kujenga Taifa mwezi Januari, 1968 na walifanya mafunzo yao katika kambi ya Ruvu iliyoko Mkoa wa Pwani.

Ili kuweka misingi bora na usimamizi bora wa uongozi, Jeshi la Kujenga Taifa lilikuwa ni Jeshi kamili kwahiyo ilipofika mwaka 1975 JKT iliunganishwa na Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania na hivyo kuwa sehemu kamili ya JWTZ.

Kuanzia wakati ule Maafisa na Askari wa JKT wakawa ni wanajeshi wa JWTZ na kutambulika kwa vyeo vya JWTZ. Kabla ya hapo JKT ilikuwa na vyeo vyake vilivyokuwa tofauti na vyeo vya JWTZ. Jeshi la Kujenga Taifa liliendelea na majukumu yake ya kutoa mafunzo kwa vijana wa kujitolea kwa mujibu wa sheria. Hata hivyo, mambo mawili ya msingi yalisisitizwa au kuongezwa katika majukumu ya JKT, kwanza JKT kuwa Divisheni ya uzalishaji ya JWTZ yenye dhamana ya kulipatia Jeshi mahitaji yake ya chakula, mavazi na mengineyo. Pili JKT ndipo mahali pa kutolea mafunzo ya awali ya kijeshi na kwamba JWTZ litaendelea kuajiri kutoka wahitimu wa JKT.

Katika dhamira ya kutimiza wajibu wa kwanza kwa ufanisi mwaka 1982 Shirika la Uzalishaji Mali la JKT (SUMA JKT) liliundwa. Shabaha kuu ilikuwa ni kuwa na chombo madhubuti cha kupanga, kusimamia, kuratibu na kutekeleza majukumu ya uzalishaji mali na kiuchumi katika JKT kazi ambayo shirika linaendelea kuifanya hadi sasa.

Kwa upande wa mafunzo kwa vijana, kwa mfano, zaidi ya vijana 305,625 wamepitia JKT na kupatiwa mafunzo ya kijeshi na stadi mbalimbali za maisha katika fani na nyanja mbalimbali. Miaka ya tisini hali ya utoaji wa mafunzo kwa vijana katika JKT iliathirika. Upatikanaji wa huduma na mahitaji kwa ajili ya mafunzo na uwezo wa kuendesha kambi za JKT kwa jumla ukawa mgumu.

Kuyumba kwa uchumi duniani, kulipelekea kupanda sana kwa bei ya mafuta, kuanguka kwa bei za mazao yaliyokuwa yanazalishwa hapa Tanzania na gharama kubwa ya vita dhidi ya majeshi ya Nduli Idi Amin wa Uganda ndivyo vilivyosababisha uchumi wa nchi yetu kutetereka. Hali hii ilipunguza sana uwezo wa Serikali kutimiza majukumu yake ya msingi katika sekta mbalimbali nchini.

Kurejeshwa kwa Mafunzo ya JKT kwa Mujibu wa sheria

Kurejeshwa kwa mafunzo ya JKT kwa mujibu wa sheria ilikuwa ni moja ya mambo yaliyopewa kipaumbele cha juu katika awamu ya nne ya serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania chini ya Amiri Jeshi Mkuu na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete. Serikali ya awamu ya nne imerudisha mafunzo ya JKT kwa sababu ya nia njema ya kuendelea kujenga uzalendo kwa vijana wa Tanzania. Itakumbukwa kwamba kutokana na hali ngumu ya kiuchumi serikali ilishindwa kumudu kuendesha mafunzo ya JKT kwa mujibu. Mnamo Juni 15, 1994 mafunzo ya JKT kwa mujibu wa sheria yalisitishwa kwa muda.

Jeshi la Kujenga Taifa limefanya kazi kubwa na nzuri ya kujenga moyo wa utaifa na uzalendo miongoni mwa vijana waliopitia katika Jeshi hilo. Hapa ni mahali ambapo vijana wa itikadi zote, rangi zote, makabila yote, dini zote hukutana, kuishi pamoja na kufanya mafunzo na kazi kama ndugu wa familia moja.

Hakuna chombo chochote cha malezi ya vijana kilichoizidi JKT katika kazi hiyo, pengine hata ile tabia ya Watanzania wengi kutoulizana makabila yao inatokana na uwepo wa JKT. Vijana wazalendo wa Tanzania wanaopitia JKT huwa wanakutana na vijana mbalimbali kutoka kila kona ya nchi yetu, ndiyo maana hawana muda hata wa kuulizana makabila kwa vile wote hujiona ni wamoja.

Aidha, athari za kusimamishwa kwa mafunzo ya JKT kuliwagusa wengi na ndiyo maana Serikali ya awamu ya nne imerejesha mafunzo ya JKT kwa mujibu wa Sheria. Hatimaye tarehe 26 Machi 2013 mafunzo ya JKT yalianza ikiwa ni pamoja na kutimiza ahadi ya serikali ya kufufua upya mafunzo hayo katika kambi ya Ruvu.

Kama ilivyokuwa mwaka 1964 JKT ilipoanza na mwaka 1968 baada ya mafunzo ya mujibu wa Sheria kuanzishwa viongozi wa kitaifa waliongoza katika kushiriki mafunzo hayo. Mafunzo hayo ya JKT yalianza na kulikuwa na idadi ya wabunge 22 ambao walishiriki na kumaliza mafunzo ya uongozi. Wabunge hao walitawanywa katika kambi mbalimbali kwa ajili ya mafunzo ya muda wa miezi miwili waliyoomba wenyewe kwa ajili ya kupata mafunzo ambayo wanaamini yatawajengea uzalendo zaidi kwa taifa lao.

Wabunge waliofanya mafunzo ya JKT baada ya kurejeshwa

Kambi ya JKT Ruvu wabunge tisa walihitimu akiwemo, Mhe. Mendrad Lutengano Kigola (MB), Mhe. David Ernest Silinde (MB), Mhe. Easter Amos Bulaya (MB), Mhe. Murtaza Mangungu (MB), Mhe. Yusuph Haji Khamis (MB), Mhe. Neema Mgaya Hamis (MB), Mhe. Halima James Mdee (MB), Mhe. Livingstone John Lusinde (MB) na Mhe. Said Mohamed Mtanda (MB).

Aidha, Wabunge watano walihitimu katika kambi ya Bulombora-Kigoma, ambao ni pamoja na Mhe Sabreena Sungura (MB), Mhe Seleman Said Jafo (MB), Mhe Mariam Kasembe (MB), Mhe Mariam Salum Msabaha (MB) na Mhe Yahaya Kasim Issa (MB). Wabunge watano walikuwa katika Kambi ya JKT Mgambo-Tanga, ambapo waliohitimu ni pamoja na Mhe Zitto Z. Kabwe (MB), Mhe Raya Khamis (MB), Mhe Dr. Anthony G. Mbassa, Mhe Idd Azzan (MB) na Mhe Abdallah Hajji Alli (MB). Kambi ya Msange mkoani Tabora nayo ilikuwa na Wabunge watatu ambao ni, Mhe Meshack Mfukwa, Mhe Rita Kabati na Mhe Mwigulu Lameck Nchemba.

Mkuu wa JKT aliopo na waliopita

Meja Jenerali Rajabu Mabele Mkuu wa JKT kuanzia tarehe 19 May 2021 hadi sasa , Brigedia Jenerali Charles Mbuge Mkuu wa JKT kuanzia Sep 2019 hadi alipopandishwa cheo kipya kuwa Meja Jenerali tarehe 02 Jun 2020 na kuendelea kuongoza Kamandi hiyo hadi tarehe 15 May 2021, Meja Jenerali Martin Busungu Mkuu wa JKT kuanzia Feb 2018 hadi Sep 2019, Meja Jenerali Michael Isamuhyo Mkuu wa JKT kuanzia Feb 2016 hadi Jan 2019 , Meja Jenerali Raphael Muhuga Mkuu wa JKT kuanzia Mar 2012 – Jan 2016 ,Luteni Jenerali Samweli Ndomba Mkuu wa JKT Mar 2012 – Sept 2012 , Meja Jenerali Samwel Kitundu Mkuu wa JKT kuanzia Sept 2008- Jan 2012 ,Meja Jenerali Martin Madata Mkuu wa JKT kuanzia Sept 2007- Sept 2008 , Meja Jenerali Abdulrahman Shimbo Mkuu wa JKT kuanzia Juni 2006 – Sept 2007 , Meja Jenerali Davis Mwamunyange Mkuu wa JKT kuanzia Oct 2001 – Juni 2006 , Meja Jenerali Makame Rashidi Mkuu wa JKT kuanzia Jan 1989 – Oct 2001 , Meja Jenerali Nelson Mkisi Mkuu wa JKT kuanzia Jan 1973 – Jan 1989 , ASP Laurence Gama Mkuu wa JKT kuanzia Mei 1970 – Jan 1973 , ASP Robert Kaswende Mkuu wa JKT kuanzia Mei 1967 –Mei 1970 , ASP David Nkulila Mkuu wa JKT kuanzia Julai 1963 – Dec 1967